Description
"Tutawaonyesha ishara Zetu katika upeo wa macho na ndani ya nafsi zao hadi iwafunulie kwamba huo ni ukweli." (Qur'an 41:53)
Kijitabu hiki kinaelezea mtazamo wa Kiislamu kuhusu kuamini Mungu. Kinaelezea jinsi Mwenyezi Mungu anavyotoa ishara za uwepo Wake - kupitia uumbaji wa asili na kupitia ufunuo, na kufafanua maswali ya kawaida ya wafuasi wa kutoamini mungu.
Mwenyezi Mungu anatuita tumtambue kupitia ishara Zake na ameifanya kuwa jukumu letu kutafakari na kufikiri ili tumtambue. Wengine wanapokea ishara hizi na kuona kazi ya Mwenyezi Mungu kila mahali, wakati wengine wanakataa kila kitu kama cha kubahatisha na kisicho na maana. Mwenyezi Mungu ameweka ndani ya kila mtu mwelekeo wa asili wa kuamini, lakini mwelekeo huu wa imani wa asili unaweza kulelewa au kukandamizwa.
Muhimu ni kwamba , Mwenyezi Mungu huwaongoza watu walio na nia safi na wanaotaka kupokea mwongozo. Kwa maneno mengine, wale wasiotaka kumwamini Mwenyezi Mungu hawataongozwa.
Mwenyezi Mungu anasema, “Mungu humwongoza kwake yeyote anayemgeukia.” (Qur’an 13:27)
Hii inahitaji kuwa na mtazamo wa kiadilifu na usio na upendeleo kuhusu uwezekano wa kuwepo kwa Mwenyezi Mungu, jambo ambalo linaweza kuwa gumu na la kunyenyekesha kwa baadhi ya watu, lakini bila uwazi na nia ya kweli, hakuna kiasi cha taarifa kinachoweza kumfanya mtu kuamini. Kwa hakika, Mwenyezi Mungu anatutahadharisha kuwa wale wanaokaribia ishara Zake kwa kiburi na majivuno wataona tu sababu ya kutoamini kwao.
Kwa hivyo, tunatarajia kwamba wale walio na nia safi, akili wazi, na wanaotafuta ukweli kwa dhati watafaidika na taarifa hizi na kwamba zitasaidia kutoa mtazamo mpya wa kumwelewa Mwenyezi Mungu.
Ni muhimu pia kutambua kwamba kutokana na tofauti kubwa kati ya Uislamu na Ukristo, ukosoaji mwingi wa Ukristo hauhusiani na Uislamu.
Sababu za Kuamini
Zifuatazo ni sababu tatu za kimantiki za kuamini Muumba.
1. Mwanzo wa Ulimwengu
Ushahidi wa kwanza unaoashiria uwepo wa Muumba unahusiana na kuelewa asili ya ulimwengu.
Fikiria unatembea jangwani na unapata saa. Tunajua kuwa saa inajumuisha kioo, plastiki na chuma.
Kioo hutoka kwa mchanga, plastiki kutoka kwa mafuta, na chuma kutoka ardhini - vipengele vyote hivi vinapatikana jangwani. Je, utaamini kuwa saa ilijitengeneza yenyewe? Kwamba jua liliangaza, upepo ukavuma, radi ikapiga, mafuta yakabubujika juu na kuchanganyika na mchanga na chuma, na baada ya miaka mamilioni saa ikajikusanya kwa bahati nasibu au matukio ya kiasili?
"Je, waliumbwa kutoka kwa bure, au walijiumba wenyewe?" (Qur'an 52:35-36)
Kulingana na sayansi ya kisasa, ulimwengu una mipaka na una mwanzo.
Ulimwengu hatimaye ulitoka wapi? Uzoefu wa kibinadamu na mantiki rahisi hutufundisha kuwa kila kitu kilicho na mwanzo hakiwezi kutokea kutoka kwa bure, wala hakiwezi kujiumba chenyewe. Tunaweza kufikia hitimisho kwamba kiumbe wa juu aliyeumba ulimwengu. Kiumbe huyu lazima awe mwenye nguvu na akili kwa kuwa ndiye aliyeleta ulimwengu mzima katika uwepo na kuweka "sheria za sayansi" zinazoutawala. Tunaweza pia kufikiri kwamba kiumbe huyu hana muda wala nafasi, kwa sababu muda, nafasi na vitu vilianza wakati wa uumbaji wa ulimwengu. Sifa hizi zote zinaunda dhana ya msingi ya Mwenyezi Mungu, Muumba wa ulimwengu.
Wengine wanaweza kuuliza, "Nani alimuumba Mwenyezi Mungu?"
Mwenyezi Mungu, Muumba, ni tofauti na viumbe vyake. Tofauti na ulimwengu na viumbe vingine vyote, Mwenyezi Mungu ni wa milele, daima amekuwepo na hana mwanzo.
2. Ukamilifu wa Ulimwengu
Ushahidi wa pili wa Muumba ni utaratibu na uwiano kamili wa ulimwengu wetu mgumu.
Je, ulimwengu mkubwa na mgumu unaweza kuundwa kwa bahati nasibu, bila usimamizi?
Vipengele vingi vya ulimwengu vinaonyesha wazi kuwa umetengenezwa mahsusi kuunga mkono maisha, kama vile umbali wa dunia kutoka kwa jua; unene wa ganda la dunia; kasi ya mzunguko wa dunia; asilimia ya oksijeni katika anga; na hata mwelekeo wa dunia. Kama vipimo hivi vingekuwa tofauti kidogo na vilivyo sasa, maisha yasingekuwepo.
Kama vile saa inavyokuwa na mtengenezaji mwenye akili wa kuweka wakati sahihi, vivyo hivyo dunia lazima iwe na mtengenezaji mwenye akili wa kuweka wakati sahihi kuzunguka Jua. Je, hili linaweza kutokea lenyewe?
Tunapoona mpangilio, sheria na mifumo sahihi ndani yetu na ulimwenguni kote, si busara kusema kwamba hakuna mpangaji? Mpangaji huyu anaelezewa vyema na uwepo wa Mwenyezi Mungu - ndiye aliyeleta mpangilio huu.
Inapaswa kufahamika kuwa Uislamu unahimiza utafiti wa kisayansi na tafakuri. Jukumu la sayansi linatusaidia kuelezea mifumo mingi inayozingatiwa ambayo Mwenyezi Mungu ameweka katika uumbaji Wake na kuthamini ukubwa wa nguvu na hekima Zake. Maendeleo katika uvumbuzi wa kisayansi, kama vile utaratibu au mchakato wowote tunaoupata katika dunia ya asili kama mzunguko wa maji au mvuto - yanatoa ishara za kuwepo kwa mpangaji na mbunifu, si hoja dhidi ya Mwenyezi Mungu.
3. Ufunuo kutoka kwa Mwenyezi Mungu
Ushahidi wa tatu ni ufunuo halisi ambao Mwenyezi Mungu ameutuma kwa wanadamu kama ishara ya uwepo Wake.
Moja ya madhumuni makuu ya kitabu cha Uislamu, Quran, ni kuita watu kutafakari na kuthamini uumbaji wa Mwenyezi Mungu kama njia ya kumuamini. Katika Quran, Mwenyezi Mungu anatuita tuangalie miundo Yake ya ajabu na ugumu wake katika ulimwengu na ndani yetu, ambavyo vinatosha kuonyesha kwamba sisi ni zao la muundo, kusudi na akili. Kwa mfano, Mwenyezi Mungu anasema:
"Hakika katika uumbaji wa mbingu na ardhi, na tofauti ya usiku na mchana, na meli kubwa zinazovuka bahari kwa manufaa ya watu, na yale ambayo Mwenyezi Mungu ameteremsha kutoka mbinguni ya mvua, kisha kufufua nayo ardhi baada ya kufa kwake, na kutawanya humo kila kiumbe kinachosonga, na mwelekeo wake wa upepo na mawingu yanayodhibitiwa kati ya mbingu na ardhi, kuna ishara kwa watu wenye akili." (Quran 2:164)
Zaidi ya hayo, kuna ishara wazi kwamba Quran ni maneno ya Mwenyezi Mungu
Qurani:
· Haina makosa wala migongano.
· Imehifadhiwa neno kwa neno tangu kufunuliwa kwake kwa lugha ya Kiarabu ya asili, tofauti na maandiko mengine.
· Quran inahifadhiwa kichwani na mamilioni ya watu kote duniani kwanzia mwanzo mpaka mwisho.
· Ina ujumbe rahisi, safi na wa ulimwengu wote unaovutia akili ya mwanadamu na imani zake za kiasili kuhusu Mwenyezi Mungu.
· Ina zaidi ya miaka 1400 na ina ukweli mwingi wa kisayansi ambao haukujulikana kwa watu wa wakati huo na umegunduliwa tu hivi karibuni na wanasayansi.
· Mifano ni pamoja na: maji kuwa asili ya viumbe vyote hai (Quran 21:30); upanuzi wa ulimwengu (Quran 51:47); na mizunguko ya jua na mwezi (Quran 21:33).
· Inayo ukweli mwingi wa kihistoria ambao haukujulikana kwa watu wa wakati huo, pamoja na unabii mwingi uliothibitishwa kuwa sahihi.
· Quran ina athari ya kina na ya kuathiri watu.
· Ilifunuliwa kwa Mtume Muhammad (amani iwe juu yake) ambaye alijulikana kuwa hajui kusoma na kuandika, lakini ina mtindo wa kipekee wa lugha unaojulikana ulimwenguni kuwa kilele cha ufasaha wa Kiarabu na uzuri wa lugha.
Maelezo ya busara zaidi kwa vipengele vingi vya kipekee na vya kimuujiza vya Quran ni kwamba hainaweza kuwa tu isipokuwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Maswali Kuhusu Mwenyezi Mungu
"Kwa nini Mwenyezi Mungu alituumba?"
Kila mtu anakubali kwamba sehemu za miili yetu, kama vile macho yetu, masikio, akili na mioyo, zina kusudi. Je, haingekuwa na maana kusema kuwa mtu binafsi pia ana kusudi?
Mwenyezi Mungu, Mwenye Hekima na elimu Yote, hakuumba sisi tu kutangatanga bila mwelekeo au kutimiza tu silika na matamanio yetu ya msingi. Badala yake, Mwenyezi Mungu anaelezea maisha haya kama mtihani. Kila mtu anajaribiwa kuhusu nani atakayechagua kumtambua Mwenyezi Mungu na kufuata mwongozo wake. Mwenyezi Mungu anasema:
"Hakika, Tumemuumba mwanadamu ... ili Tumjaribu; na Tumempa masikio na macho. Hakika, Tumemwonyesha njia, iwe atashukuru au atakufuru." (Quran 76:2-3)
Kwa wengi, suala la msingi si kuhusu kumuamini Mwenyezi Mungu, bali kuhusu athari za kumuamini Yeye.
Hii itamaanisha kuwajibishwa na kuhukumiwa kwa matendo yao, jambo ambalo linaweza kuwa kero kwa maisha wanayotaka kuishi.
Kwa hivyo, mtihani wa maisha haya ni kufuata na kujinyenyekeza mbele ya Mwenyezi Mungu badala ya kufuata matamanio, kiburi na ubinafsi wetu.
"Kwa nini Mwenyezi Mungu anahitaji kutujaribu?"
Mwenyezi Mungu hahitaji chochote - Hahitaji kuumba chochote wala hahitaji kumjaribu mtu yeyote.
Yeye hanufaiki na imani yetu wala haathiriki na ukafiri wetu. Bali, ni sehemu ya hekima Yake isiyo na mipaka kwamba alituumba na kutupa nafasi ya kujijua. Mwenyezi Mungu anajua yajayo - dhumuni ni sisi kuishi maisha yetu, kuyapitia na kufanya maamuzi yetu wenyewe.
"Je, tunayo kweli chaguo?"
Ukweli kwamba Mwenyezi Mungu anajua chaguo zetu hauifanyi kuwa chini ya hiari. Ingawa Mwenyezi Mungu anataka watu wamuamini Yeye, ingawa Yeye hamlazimishi mtu yeyote. Kama Mungu angelipenda, Angewaongoza wanadamu wote, kwa kuwa ana uwezo juu ya kila kitu. Lakini kwa Hekima Yake, alituumba na uwezo wa kuchagua na kutufanya wawajibikaji kwa chaguo zetu. Mwenyezi Mungu haridhiki kila wakati na kila kitu anachoruhusu kitokee.
"Kwa nini Mwenyezi Mungu haonekani moja kwa moja?"
Kwa hekima Yake, Mwenyezi Mungu amechagua kujitambulisha kupitia ishara Zake. Hili ni sehemu ya mtihani wa maisha haya.
Ametufanya kuwajibika kutumia uwezo alio tupatia ili kumtambua Yeye. Hii inamaanisha kwamba ni wale tu ambao ni waaminifu, wanyenyekevu, na wanaotafakari kwa kina ndio watamjua na kumwamini Mwenyezi Mungu.
"Kwa nini kuna mateso duniani?"
Ukweli kwamba watu wanapimwa kwa njia tofauti kupitia majaribu mbalimbali haukanushi kuwepo kwa Mwenyezi Mungu wala kupingana na kuwa kwake mwenye nguvu zote.
Badala yake, mazuri na mabaya ambayo Mwenyezi Mungu anaruhusu kutokea ni sehemu ya mtihani wetu duniani. Hatuwezi kudhibiti kile kinachotutokea, lakini tunaweza kudhibiti jinsi tunavyoitikia, na hapo ndipo Mwenyezi Mungu anatupimia. Dunia hii ni ya kupita na isiyo thabiti, lakini haki kamili katika akhera, ambayo ni ya milele, itafidia zaidi dhuluma au mabaya yoyote ya maisha haya.
"Kwa nini Mwenyezi Mungu anawaadhibu watu?"
Hakuna mtu anayeweza kupinga dhana ya adhabu, ambayo ni muhimu kwa ajili ya uadilifu. Mwenyezi Mungu ametuumba na uwezo wa kuchagua jinsi tunavyotaka kuishi, na kwa hivyo, kuwajibika.
Wale wanaojitahidi kwa dhati kumtii Mwenyezi Mungu watapata rehema yake na kuingia Peponi.
Lakini wale wanaopuuza lengo lao la maisha na kukanusha uwepo wa Mwenyezi Mungu, hatimaye wamefanya uchaguzi wao wenyewe na watawajibika. Hakuna mtu anayeweza kumlaumu Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu hakuumba watu ili kuwaadhibu – bali, anakusudia kuwafanyia urahisi na kuwapa rehema. Ukweli kwamba Mwenyezi Mungu anajua uchaguzi wetu haufanyi matendo yetu kuwa yasiyo ya hiari, wala haitutoi katika uwajibikaji.
Uislamu ni dini ya vitendo inayohimiza usawa kati ya matumaini ya rehema ya Mwenyezi Mungu na hofu ya adhabu Yake - zote zinahitajika kuishi maisha chanya na ya unyenyekevu. Mwenyezi Mungu ni Mwenye Rehema lakini pia Mwenye Haki zaidi. Ikiwa hakutakuwa na Siku ya Hukumu, itapingana na haki kamilifu ya Mwenyezi Mungu, na maisha yatakuwa si ya haki.
Hitimisho
Je, tuko hapa kwa miaka 80 tu au zaidi, na ndiyo yote? Au kuna zaidi ya maisha?
Je, sisi ni sokwe waliotangamana bila lengo kuu? Je, sisi ni viumbe wa kimwili wenye mahitaji ya kimwili pekee au tuna mahitaji ya kiroho pia?
Kwa wale walio waaminifu na bado hawajapata uamuzi kuhusu Mwenyezi Mungu, ushauri wetu ni kuuliza kwa dhati yafuatayo:
"Mungu, ikiwa unapatikana, tafadhali niongoze." Unaweza kushangazwa na matokeo!
