Description
Dhana Potofu Kuhusu Uislamu
Unajua nini kuhusu Uislamu?
Utangulizi
Uislamu ni mojawapo ya dini kubwa zaidi ulimwenguni, lakini pia ni mojawapo ya dini ambazo hueleweka vibaya zaidi. Kwa sababu mbalimbali - iwe ni za kisiasa, kiuchumi, vyombo vya habari vyenye upendeleo au hofu ya "wengine" - zimesambaza uwongo na dhana potofu kuhusu Uislamu. Ufunguo wa kuelewa Uislamu na Waislamu ni kupinga dhana potofu na kuchunguza kila hali kulingana na mafundisho ya Kiislamu na vyanzo sahihi.
Dhana Potofu ya Kwanza - "Waislamu Hawashiriki Maadili Mazuri na Ya Heshima na Wasiokuwa Waislamu"
"Bora zaidi kati yenu ni wale walio na tabia bora zaidi." - Mtume Muhammad (rehema na amani zimshukie)
Baadhi ya watu hudai kwamba maadili ya Kiislamu hayaambatani kwa njia yoyote na maadili mazuri ya "Magharibi". Madai haya hayana ukweli wowote.
Waislamu wanathamini maadili ya heshima ya ulimwengu wote kama:
· Kuwa waaminifu na waadilifu
· Kutimiza ahadi
· Kuruhusu uhuru wa dini
· Kuheshimu wazazi, undugu, majirani, na wazee
· Kuwa wakarimu, wema, na kuwajali maskini na wahitaji
· Kuwajali majirani
· Kutokusema uongo, kudanganya, kutukana au kumsengenya yeyote
Waislamu wanapaswa kuchangia vyema kwa jamii na kila mara kuwa na maadili ya juu na matendo bora.
Dhana Potofu ya 2 – "Waislamu Wanamwabudu Mungu Mpya Anayeitwa Allah"
Waislamu wanamwabudu Mungu yule yule aliyekuwa akiabudiwa na Manabii Nuhu, Ibrahim, Musa na Isa.
Neno "Allah" ni neno la Kiarabu linalomaanisha Mwenyezi Mungu – neno la Kiarabu lenye maana tele, likimaanisha Mungu mmoja wa pekee. "Allah" ni neno lile lile linalotumiwa na Wakristo na Wayahudi wanaozungumza Kiarabu kumrejelea Mungu.
Hata hivyo, ingawa Waislamu, mayahudi na Wakristo wanaamini Mungu mmoja (Muumbaji), dhana zao kuhusu Yeye zinatofautiana sana. Kwa mfano, Waislamu wanakataa wazo la Mungu kuwa na washirika wowote au kuwa sehemu ya "Utatu", na wanampa Mwenyezi Mungu ukamilifu pekee.
Dhana Potofu ya 3 – "Uislamu Unaruhusu Ugaidi"
Vyombo vya habari kwa kawaida vinamwonyesha Mwislamu yeyote anayepigana kama gaidi, bila kujali ikiwa wanapigana kwa haki au kwa njia isiyo ya haki, au ikiwa wanawaonea wengine au wanaonewa.
Katika vita, kulenga watu wasio na hatia wasiopigana ni kitendo cha kuchukiza ambacho Uislamu unakataza wazi. Kwa kweli, Waislamu hawaruhusiwi kuharibu mimea na wanyama bila sababu, achilia mbali wanadamu wasio na hatia. Hata hivyo, ni muhimu kutofautisha kati ya ugaidi na upinzani halali dhidi ya uvamizi, kwani haya mawili ni tofauti kabisa.
Quran inaonyesha wazi uzito wa kuua mtu asiye na hatia, na kusisitiza thamani ya maisha ya binadamu.
"Mtu akimuua mtu asiye na hatia, ni kama amewaua wanadamu wote; na mtu akimwokoa mtu mmoja, ni kama ameokoa wanadamu wote." (Qur'an 5:32)
Dhana Potofu ya 4 – "Uislamu Unawakandamiza Wanawake"
Katika Uislamu, wanaume na wanawake wanachukuliwa kuwa sawa mbele ya Mungu, kwa kupata thawabu na uwajibikaji sawa kwa matendo yao. Kitu pekee kinachowatofautisha watu mbele ya Mungu ni kiwango chao cha uchamungu.
"Hakika mwenye kuheshimika zaidi kati yenu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule anayemcha Mungu zaidi." (Qur'an 49:13)
Aya hii inathibitisha kuwa heshima ya kweli na hadhi haipatikani kwa sababu ya utajiri au umaskini, weusi au weupe, mwanamume au mwanamke, bali kwa uchamungu na ibada.
Mwenyezi Mungu, Muumba wa jinsia zote mbili, amewapa kila mmoja majukumu tofauti kwa kuzingatia tofauti zao.
Wanawake wanapewa heshima ya hali ya juu, kama vile haki ya malipo sawa, kuchagua mwenzi wa ndoa, kufuata elimu, na haki ya talaka na urithi.
Kwa bahati mbaya, kuna wanawake Waislamu ambao wanakandamizwa na hawapewi haki zao. Hili si kosa la Uislamu. Shida ni kwamba katika baadhi ya nchi, watu hufuata desturi na mila fulani ambazo hazina uhusiano na Uislamu.
Dhana Potofu ya 5 – "Qur'an ni Kitabu Kingine tu c ha Historia au Mashairi"
Qur'an ni neno la Mwenyezi Mungu lililo halisi, lililofunuliwa kwa Mtume Muhammad (rehma na amani zimshukie) kupitia malaika Jibril. Ni kipimo cha ukweli, chenye mwongozo wa kuishi kwa wanadamu. Qur'an inatoa masomo kutoka kwa vizazi vilivyopita na historia ya Manabii ili tujifunze kutokana na uzoefu wao.
Pia inatufundisha kuhusu sisi wenyewe na Muumba wetu, pamoja na kusudi la kuwepo kwetu ambalo ni kumtambua Mungu na kumwabudu Yeye peke yake.
Mungu hakuumba wanadamu ili watembee bila lengo. Jaribio la imani ya mtu ni kutumia akili, hiari na uwezo wa kufikiria ili kutafakari na kutambua ishara za Mwenyezi Mungu - moja ya ishara kuu ikiwa ni Qur'an.
Qur'an ina miujiza mingi ndani yake, ili tusiwe na shaka juu ya ukweli wake.
Njia bora ya kugundua Qur'an inahusu nini hasa, ni kuisoma mwenyewe.
Dhana Potofu ya 6 – "Hijabu ni ya Kukandamiza"
Ili kuzingatia hijabu, wanawake Waislamu wanahitajika kufunika miili yao kwa mavazi ya heshima yasiyoonyesha maumbo yao mbele ya wanaume wasio mahram.
Hata hivyo, hijabu si kuhusu mwonekano wa nje pekee; pia inahusu usemi mzuri, unyenyekevu, na mwenendo wa heshima.
Ingawa hijabu ina faida nyingi, sababu kuu ya wanawake Waislamu kuvaa hijabu ni kwamba ni amri kutoka kwa Mwenyezi Mungu, naye anajua yaliyo bora kwa viumbe Wake.
Hijabu humwezesha mwanamke kwa kusisitiza uzuri wake wa kiroho wa ndani badala ya mwonekano wake wa nje. Inawapa wanawake uhuru wa kuwa washiriki hai wa jamii, huku wakidumisha unyenyekevu wao.
Hijabu haiashirii ukandamizaji, udhalimu au kimya. Badala yake, ni kinga dhidi ya matamshi ya kudhalilisha, majaribio yasiyotakiwa, na ubaguzi usio wa haki. Kwa hivyo wakati ujao unapomwona mwanamke Mwislamu, fahamu kwamba anafunika mwonekano wake wa nje, si akili yake wala fikra zake.
Dhana Potofu ya 7 – "Waislamu Wote ni Waarabu"
Takriban 20% tu ya Waislamu duniani ni Waarabu, ikimaanisha kuwa hadi 80% ya Waislamu si Waarabu. Kwa mfano, kuna Waislamu wa India na Indonesia zaidi ya Waislamu wa Kiarabu.
Uislamu unafundisha kwamba mtu si bora zaidi kuliko mwingine kwa sababu ya rangi au kabila, na unapingana vikali na aina yoyote ya ubaguzi wa rangi. Uislamu una ujumbe wa ulimwengu kwa wanadamu wote - kwamba kila mtu anaweza kupata amani na mafanikio kwa kumtambua na kumwabudu Mungu Mmoja wa Kweli.
Dhana Potofu ya 8 – "Jihad ni Ugaidi"
Kiini cha Jihad ni kupambana na kujitolea kwa ajili ya dini kwa njia inayompendeza Mwenyezi Mungu. Kimsingi, inamaanisha "kupambana" na inaweza kumaanisha kujitahidi kufanya matendo mema, kutoa sadaka, au kushiriki katika hatua ya kijeshi ya Kiislamu. Aina inayojulikana zaidi ni Jihad ya kijeshi ambayo inaruhusiwa ili kuhifadhi ustawi wa jamii, kuzuia ukandamizaji kuenea, na kukuza haki. Hii inaweza kuwa ya kujihami au ya kushambulia, kulingana na hali.
Dhana Potofu ya 9 – "Waislamu Wanamuabudu Muhammad au Mungu wa Mwezi"
Dhana potofu nyingine ni kwamba Waislamu wanamuabudu Mtume Muhammad (rehma na amani ziwe juu yake). Hili si kweli hata kidogo, na linaweza kukanushwa kwa urahisi kwa kauli ya Mtume (rehma na amani ziwe juu yake): "Msinisifu kupita kiasi kama vile Wakristo walivyomsifu Yesu mwana wa Mariamu. Mimi ni mja wa Mwenyezi Mungu, basi niiteni mja wa Mwenyezi Mungu na Mtume Wake."
Uislamu unawafundisha Waislamu kuwaheshimu Manabii wote wa Mwenyezi Mungu na Mitume Wake – lakini kuwaheshimu na kuwapenda haina maana ya kuwaabudu.
Dai lingine linalohusiana ni kwamba Waislamu wanamuabudu "Mungu wa Mwezi" ambalo pia si kweli kabisa. Kuabudu mwezi, au chochote isipokuwa Mwenyezi Mungu, ni marufuku kabisa katika Uislamu:
"Msisujudie jua wala mwezi, bali msujudie Mwenyezi Mungu aliyeviumba, ikiwa mnamuabudu Yeye kweli." (Qur'ani 41:37)
Uislamu unatambua ukamilifu wa hali ya juu, ukuu, na upekee wa Mwenyezi Mungu bila masharti yoyote. Yeye ni mwadilifu Zaidi na Mwenye Rehema Zaidi.
Kumuabudu Yeye peke yake ndiyo imani muhimu zaidi katika Uislamu, kama inavyotajwa katika sehemu nyingi za Qur'an.
Dhana Potofu ya 10 – "Uislamu Unaruhusu Ndoa za Kulazimishwa"
Ndoa zilizopangwa ni desturi za kitamaduni ambazo zinashamiri katika baadhi ya nchi duniani. Ingawa si ya Waislamu pekee, ndoa za kulazimishwa zimehusishwa kimakosa na Uislamu.
Katika Uislamu, wanaume na wanawake wote wana haki ya kuchagua au kukataa mwenza wao anayetarajiwa, na ndoa huchukuliwa kuwa batili ikiwa idhini ya kweli ya mwanamke haijatolewa kabla ya ndoa.
Dhana Potofu ya 11 – "Uislamu Unalazimisha Watu Kuwa Waislamu"
Mwenyezi Mungu anasema, "Hakuna kulazimishwa katika dini. Ukweli umefanywa wazi kutoka kwa makosa." (Qur'ani 2:256)
Ingawa ni wajibu wa Waislamu kufikisha ujumbe mzuri wa Uislamu kwa wengine, hakuna anayepaswa kulazimishwa kuukubali Uislamu. Ili kuukubali Uislamu, mtu lazima amwamini Mwenyezi Mungu kwa dhati na kwa hiari na kumtii, kwa hivyo, hakuna mtu anayepaswa kulazimishwa kuukubali Uislamu.
Fikiria yafuatayo:
· Indonesia ina idadi kubwa zaidi ya Waislamu lakini hakuna vita vilivyopiganwa kuleta Uislamu huko.
· Kuna takriban Wakristo 14 milioni wa Kikoptiki wa Kiarabu wanaoishi katika nchi za Uarabuni kwa vizazi vingi.
· Uislamu ni moja ya dini zinazokua kwa kasi zaidi katika ulimwengu wa magharibi leo.
· Ingawa kupambana na dhuluma na kukuza haki ni sababu halali za jihad, lakini kulazimisha watu kuukubali Uislamu si moja yao.
· Waislamu walitawala Hispania kwa takriban miaka 800 lakini hawakuwalazimisha watu kubadili dini ya uislamu.
Hitimisho
Kujifunza kuhusu Uislamu kutoka kwa vyanzo visivyostahili bila uthibitisho ni hatari na husababisha kutoelewana. Usikubali kupotoshwa kwa kukubali dhana potofu na taarifa za uongo kuhusu Uislamu – imani inayoshirikiwa na zaidi ya robo ya wanadamu.
Je, ujumbe wa Uislamu, mwongozo kwa wanadamu wote, hustahili kufikiriwa kwa makini na kutafakariwa?
