Hatari za Riba خطر الربا

3.64 MB 43 1 Files
albyan
or download free
[free_download_btn]

Description

"Enyi mlioamini! Msile riba kwa kuzidisha maradufu, na mcheni Mwenyezi Mungu ili mpate kufaulu." [Qur'an 3:130]

Utangulizi

Je, si ajabu kwamba Muislamu hatakula nyama ya nguruwe kwa sababu ni haramu; hatamuoa mama yake au dada yake kwa sababu pia ni haramu, lakini mtu huyo huyo hana tatizo la kula riba (kama vile faida au ushuru)? Je, unajua kwamba kufanya muamala kwa riba ni dhambi kubwa ambayo inaweza kukupeleka Motoni?

"...Lakini atakayerejea (kufanya riba), hao ni watu wa Moto - humo watadumu milele." [Qur'an 2:275]

Ikiwa kuamiliana kwa riba kuna adhabu kubwa, kwa nini Waislamu wengi wanaingia katika dhambi hii na kuichukulia kirahisi?

Maana ya Riba

Riba ni jina la Kiarabu lililotokana na kitenzi Raba, linalomaanisha ‘kukuza’, ‘kuongezeka’, au ‘kuzidi’. Linajumuisha riba inayolipwa na benki au mikopo kama mikopo ya magari, nyumba, au deni la kadi ya mkopo.

Dalili ya kuharamisha riba

Kuna ushahidi mwingi unaoonyesha kwamba riba ni haramu na ni miongoni mwa madhambi makubwa zaidi katika Uislamu!

Kwa wale wenye imani ya kweli kwa Mwenyezi Mungu na Qur'an, aya hii wazi inatosheleza kukataza riba:

"...Mwenyezi Mungu ameruhusu biashara na amekataza riba." [Qur'an 2:275]

Katika Qur'an, Mwenyezi Mungu hatangazi vita dhidi ya yeyote isipokuwa wale wanaoamiliana kwa riba:

"Enyi mlioamini, mcheni Mwenyezi Mungu na acheni riba iliyobaki, ikiwa nyinyi ni waumini wa kweli. Na msipofanya hivyo, basi fahamuni kuwa mtatangaziwa vita kutoka kwa Mwenyezi Mungu na Mtume Wake." [Qur'an 2:278-279]

Je, ungependa Mwenyezi Mungu, Mwenye Nguvu zote, akutangazie vita baada ya kufafanua wazi kuwa riba ni haramu?

Mtume (amani iwe juu yake) alionya kwamba kula riba ni moja ya madhambi saba yanayoangamiza mtu na kumpeleka Motoni. (Bukhari na Muslim)

Riba ni haramu katika nyanja zake zote, kama alivyosema Mtume (amani iwe juu yake) (Muslim):

"Mwenyezi Mungu amemlaani yule anayekula riba, anayetoa, mashahidi wa riba, na anayefanya maandishi ya muamala huo."

Usiwe miongoni mwa wale ambao Mwenyezi Mungu amewalaani!

Kwa Nini Riba ni Haramu?

Sababu ya kwanza na kuu kwa nini riba ni haramu ni kwa sababu Mwenyezi Mungu ameiweka hivyo. Ni kwa msingi wa hekima isiyo na mipaka ya Mwenyezi Mungu kwamba Anahukumu kitendo kuwa cha lazima au haramu, akiamuru mambo kwa manufaa ya mwanadamu katika dunia hii na Akhera, kwani Yeye ni Mwenye Hekima, Mwenye Kujua yote. Wanazuoni wa Kiislamu wamependekeza sababu zifuatazo yanayobainisha kwa nini riba ni haramu:

· Mataifa yote, makubwa na madogo, yana madeni ya kigeni makubwa kiasi kwamba malipo ya riba juu ya madeni haya yamekuwa mzigo mzito kwa nchi nzima. Deni linaua. Takribani watoto milioni 11 hufa kila mwaka duniani kote kutokana na hali za umaskini na madeni. Rais wa zamani Obasanjo alitoa maoni kuhusu deni ambalo Nigeria inakabiliana nalo:

"Yote tuliyokopa hadi 1985 au 1986 yalikuwa karibu dola bilioni 5 na tumelipa karibu dola bilioni 16, lakini bado tunaambiwa tunadaiwa karibu dola bilioni 28. Dola hizo bilioni 28 zilitokana na dhuluma ya viwango vya riba vya wakopeshaji wa kigeni. Ukiniuliza kitu kibaya zaidi duniani, nitakwambia ni riba yenye kuongezeka."
- Habari za Jubilee 2000, Agosti 2000

· Riba inapingana na roho ya udugu na huruma, na inajengwa juu ya tamaa, ubinafsi na ukatili wa moyo.

· Riba ni moja ya sababu kubwa za mfumuko wa bei.

· Riba husababisha msongo wa mawazo na huzuni kutokana na kuongezeka kwa madeni.

· Riba inaleta faida isiyo na hasara yoyote, na hivyo mzigo wa hatari unabebwa na mkopaji, badala ya kushirikisha hatari na faida kati ya pande zote mbili.

· Riba inaunda ukiritimba katika jamii, ambapo matajiri wanapewa tuzo kwa utajiri wao, huku maskini wakilazimishwa kulipa zaidi!

Wakati wa mgogoro wa kifedha wa kimataifa mwaka 2008 na 2009, gazeti la kila siku la Vatican, L’Osservatore Romano, liliripoti kuwa Vatican ilisema mfumo wa kifedha wa Kiislamu unaweza kusaidia benki za Magharibi katika mgogoro kama mbadala. Vatican ilishauri: "Kanuni za kimaadili ambazo mfumo wa kifedha wa Kiislamu umejengwa juu yake zinaweza kuzileta benki karibu na wateja wao na kwa roho ya kweli ambayo inapaswa kuashiria kila huduma ya kifedha."

Pale ambapo soko la riba linaposhindwa, taasisi za kifedha za Kiislamu hazipati madhara sawa kwa sababu hatari inagawanywa kati ya pande zote mbili. Wakopeshaji watakuwa waangalifu zaidi, kwani wanashiriki hatari ya kupoteza fedha ikiwa mkopaji hawezi kurudisha kiasi cha asili.

Kwa kuzingatia matatizo yote ambayo riba inaleta, si ajabu kwamba Uislamu unakataza kitendo hiki cha kuchukiza.

Ninawezaje Kuepuka Riba?

Kuishi katika jamii ya kibepari kunafanya kuwa vigumu kuepuka riba kabisa. Hata hivyo, hili halipaswi kutumika kama kisingizio cha kuendelea kushiriki ndani yake. Njia iliyo wazi ya kuepuka uovu huu ni kutokuchukua mkopo unaohusisha malipo ya riba. Suluhisho zingine ni pamoja na:

· Kufungua akaunti za benki zisizo na riba.

· Kutokuingia katika mikataba inayolazimisha adhabu ya riba, hata kama unakusudia kulipa kwa wakati.

· Kufanya malipo ya bili kwa wakati ili kuepuka adhabu ya kuchelewa.

· Kutimiza masharti yoyote yanayohitajika ili kuendelea na biashara bila kutumia riba.

· Kukopa pesa kutoka kwa familia au marafiki pale inapowezekana.

· Kuamiliana na benki zinazozingatia sheria za Kiislamu.

· Kupanga nyumba ikiwa huwezi kumudu kununua bila riba.

· Kukubali au kupanga “mkopo mwema” (al-qard al-hasanah), ambao ni mkopo unaokusudia kuonyesha wema kwa mwingine bila riba.

Kuhusu riba ambayo benki imekupa, usiirudishe wala kuitumia. Badala yake, itumie kwa mambo ya sadaka, kama kuwapa masikini, kununua vitu vinavyotumika (kama karatasi za choo) kwa vituo vya Kiislamu na misikiti, au kusaidia wenye madeni. Hata hivyo, usitarajie malipo kwa ajili ya hili.

Njia bora zaidi ya kuepuka riba ni kuainisha miamala gani inayoruhusiwa kwa kushauriana na wanazuoni wa Kiislamu na kutumia elimu yao.

Je, Ikiwa Nimefikia Hali ya Uhitaji?

Katika Uislamu, mtu husamehewa kufanya kitendo kilichokatazwa wakati wa dharura kubwa.

Kwa hivyo, ikiwa mtu amelazimika kutumia riba, vinginevyo akabiliwe na mateso makubwa au kifo, riba inaruhusiwa kwa muda, mpaka hali hiyo ipite.

Kumbuka kuwa kuvumilia mateso yanayotokana na kujiepusha na riba, kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, kutapata thawabu.

Mtu mwenye elimu ya Kiislamu na uelewa wa hali ya kibinafsi ndiye anayepaswa kuamua ikiwa mtu yuko katika dhiki kweli.

Vinginevyo, upendeleo huu wa kanuni unaweza kutumiwa vibaya, na watu wengi wanaweza kutumia riba kimakosa na kuathiriwa na matokeo yaliyowekwa na Mwenyezi Mungu.

Kuna dhana potofu ya kawaida miongoni mwa Waislamu kuhusu kununua nyumba ya kwanza kwa kutumia riba. Wengine wanadai kuwa ni halali, wakisema ni “dharura.”

Ukweli kwamba mtu anaweza kupanga nyumba kwa urahisi badala ya kuinunua, unathibitisha kwamba dai hili si sahihi. Ikiwa nadharia hiyo ni kweli, je, inamaanisha kunywa chupa ya kwanza ya pombe ni halali ilhali maji yapo? Au kula nyama ya nguruwe wakati mbadala wa halali upo? Inaweza kuwa rahisi kuwahadaa wengine kuamini hili, lakini tunapaswa kukumbuka kwamba:

"...Mwenyezi Mungu anajua mnayoyadhihirisha na mnayoyaficha." [Qur'an 5:99]

Kulipa kodi ya nyumba ili kujikimu na kusaidia familia si “pesa zilizopotea.”

Mwenyezi Mungu Mwenye Shukrani, atalipa hili kama sadaka: InshaAllah, "mtu Anapomgharimia familia yake kwa kutarajia thawabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu, basi hilo linahesabiwa kuwa sadaka kwake." (Bukhari na Muslim)

Mafanikio Katika Dunia Hii na Akhera

Tunapochunguza suala la riba, tunapaswa kukumbuka kwamba mafanikio ya kweli yapo kwa msaada wa Mwenyezi Mungu pekee. Tukifuata yaliyo halali na kuepuka yaliyo haramu, mali yetu itabarikiwa na kuwa na manufaa katika dunia hii na Ak hera. Kuna faida gani ya pesa ya ziada inayopatikana kupitia riba ikiwa haina baraka na imelaaniwa - chanzo cha mateso?

Siku ya Kiyama, watu watafufuka kutoka makaburi yao kwa haraka, isipokuwa wale walioshiriki katika riba. Watasimama kisha wataanguka chini kama wenye kifafa kwa sababu:

"Wale wanaokula riba hawatasimama (Siku ya Kiyama) isipokuwa kama anavyosimama ambaye amepagawa na Shetani kwa wazimu. Hayo ni kwa sababu wanasema, 'Biashara ni kama riba.' Lakini Mwenyezi Mungu ameruhusu biashara na amekataza riba..." [Qur'an 2:275]

Hiyo ndio Adhabu ya wale wanaokula riba na hawatubu kwa dhati kutokana na dhambi hili kubwa ndivyo ilivyo.

Kwa wale wanaojitahidi kufanikisha mafanikio kwa kupata radhi za Mwenyezi Mungu, wanapata faraja kutoka aya ifuatayo:

"Enyi mlioamini! Msile riba kwa kuzidisha maradufu, na mcheni Mwenyezi Mungu ili mpate kufaulu." [Qur'an 3:130]

Tunafundishwa pia jinsi ya kufanikiwa Akhera:

"Hakika usemi wa waumini wanapoitwa kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake ili ahukumu baina yao ni kusema: ‘Tumesikia na tumetii.’ Na hao ndio wenye kufaulu (watakaokaa milele Peponi)." [Qur'an 24:51]

Hitimisho

Hakuna shaka kwamba riba ni haramu na ni dhambi kubwa, na hakuna uasi wa Mwenyezi Mungu unaostahili hatari ya adhabu Yake. Tunapaswa kukumbuka kuwa maisha ya dunia hii ni mafupi na ya kupita, na kwamba lengo la kuwepo kwetu si kufuata uzuri na mali, bali ni kumwabudu Mwenyezi Mungu kama ipasavyo na kuishi kwa sheria Zake. Kwa sababu tu riba imeenea na kuwa jambo la kawaida, haimaanishi kuwa ni halali.

"Na anayemcha Mwenyezi Mungu, Atamtengezea njia ya kutoka (katika kila shida), na Atamruzuku kutoka pale asipotarajia. Na anayemtegemea Mwenyezi Mungu, basi Yeye humtosheleza." [Qur'an 65:2-3]

Similar Downloads

No related download found!