Unabii Katika Uislamu النبوة في الإسلام

3.65 MB 114 1 Files
albyan
or download free
[free_download_btn]

Description

Unabii Katika Uislamu

Nuhu, Ibrahimu, Musa, Yesu, Muhammad

Amani Iwe Juu Yao

Allah (Mwenyezi Mungu), Muumba wa ulimwengu na vyote vilivyomo, aliwaumba wanadamu kwa lengo tukufu: kumuabudu Yeye pekee na kuishi maisha ya wema kulingana na mafundisho na mwongozo Wake.

Hata hivyo, haiwezekani kutimiza lengo hili bila kupokea mwongozo wa wazi kutoka kwa Allah.

Allah, Mwingi wa Rehema na Haki, hakutuacha tuzunguke duniani bila lengo. Ili kutufahamisha kusudi letu, Allah aliteua watu maalumu kufikisha na kuonyesha ujumbe Wake kwa wanadamu wote. Watu hawa wanajulikana kama Manabii, wakiwemo Adamu, Nuhu, Ibrahimu, Musa, Yesu na Muhammad – amani iwe juu yao wote.

Sifa za Manabii

Manabii wote wana sifa zinazowafanya kuwa wanadamu wa kipekee.

Manabii hupokea ufunuo

Tofauti kuu kati ya mwanadamu wa kawaida na Nabii ni kwamba Nabii hupokea ufunuo kutoka kwa Allah.

Manabii wana tabia tukufu

Manabii hawakutafuta faida binafsi kama vile mali, cheo cha juu au mamlaka – badala yake walitafuta tu radhi za Mungu.

Manabii walikuwa mifano bora kati ya watu wao kwa tabia njema na ucha-Mungu. Waliishi kwa kumtii Mwenyezi Mungu, wakiwa na maadili mema na walikuwa wakweli daima kwa maneno na matendo. Kwa sababu hii, Waislamu wanakataa kabisa madai ya uwongo ya kuwahusisha Manabii na madhambi makubwa kama inavyoonekana katika maandiko ya dini nyingine.

Manabii hufanya miujiza

Manabii wengi walifanya miujiza, mara nyingi katika uwanja ambao watu wao walibobea. Kwa mfano, watu wa Musa (amani iwe juu yake) walibobea katika uchawi; kwa hivyo, Musa (amani iwe juu yake) aliweza kufanya matendo ya miujiza ambayo hata wachawi hawakuweza kuyafanya. Watu wa Isa (amani iwe juu yake) walibobea katika masuala ya tiba; kwa hivyo, Isa (amani iwe juu yake) aliweza kufanya matendo ya uponyaji yaliyokuwa zaidi ya ujuzi wa watu wake. Watu wa Muhammad (rehma na amani iwe juu yake) walibobea katika ushairi; kwa hivyo, Muhammad (rehma na amani iwe juu yake) alileta Quran, yenye maneno fasaha ambayo hakuna mshairi aliyewahi kuyashinda. Zaidi ya hayo, Manabii wengi walitoa unabii wa kweli wa matukio yajayo. Miujiza hii ilifanyika tu kwa idhini na msaada wa Allah, ikithibitisha kwamba walikuwa wanadamu, si miungu.

Manabii si Miungu

Ingawa Manabii wamechaguliwa na Allah Mtukufu, hawana uungu wowote na hawapaswi kuabudiwa. Mtume Muhammad (rehma na amani iwe juu yake) aliagizwa kusema:

"Mimi ni mwanadamu tu kama nyinyi. Imenifunuliwa kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja." Qur'an 18:110

Ni dhahiri hata katika Biblia, Agano la Kale na Jipya, kwamba Manabii hawakuwa miungu, na walikuwa wakimuabudu na kumsujudia Mwenyezi Mungu Mmoja wa Kweli.

"Naye [Yesu] alienda mbele kidogo, akajitupa kifudifudi, na kuomba..." Mathayo 26:39

"Nao [Musa na Haruni] walianguka kifudifudi..." Hesabu 16:22

"Na Abramu [yaani Ibrahimu] alianguka kifudifudi, naye akazungumza Mungu ..." Mwanzo 17:3

Ujumbe wa Manabii

"Hakika Tulituma kwa kila taifa Mjumbe (akisema): ‘Muabuduni Allah na jiepusheni na miungu ya uongo.’" Qur’an 16:36

Kwa kuwa Manabii wote walitumwa na Mwenyezi Mungu Mmoja wa Kweli, walifikisha ujumbe ule ule na walikuwa na dhamira moja – kukumbusha na kuwafundisha watu wao kusudi la maisha.

Ujumbe wao ulikuwa:

· Kufafanua dhana ya kweli ya Mwenyezi Mungu na kukataa imani za uongo

· Kufundisha kusudi la kweli la maisha

· Kuonyesha jinsi Allah anavyopaswa kuabudiwa

· Kufikisha tafsiri ya Allah ya mwenendo mwema na baya, na kuwashauri watu ipasavyo

· Kueleza thawabu za utiifu (Peponi) na kuonya adhabu ya uasi (Motoni)

· Kufafanua masuala yanayokosewa kueleweka kama roho, malaika na pepo, siku ya mwisho na kadari

"Na hatukutuma Mjumbe yeyote isipokuwa kwa lugha ya watu wake, ili awafafanulie..." Qur'an 14:4

Lengo kuu la Manabii wote lilikuwa kufafanua dhana ya Mwenyezi Mungu: kwamba Hana mshirika au anayefanana Naye, na ibada yote inapaswa kuelekezwa Kwake pekee. Katika Qur'an, kuna mifano mingi ya Manabii waliotangaza ujumbe huu:

Nuhu (amani iwe juu yake) alisema [Qur'an 7:59],

"Enyi watu wangu! Muabuduni Allah! Hamna miungu mingine isipokuwa Yeye."

Ibrahimu (amani iwe juu yake) alisema [Qur'an 21:66],

"Je, mnaabudu badala ya Allah, vitu ambavyo havikuleteeni faida wala madhara?"

Musa (amani iwe juu yake) alisema [Qur'an 7:140],

"Je! Nitamtafutia Mwenyezi Mungu mwingine badala ya Allah, ilhali Yeye amewafadhilisha juu ya viumbe vyote?"

Isa (amani iwe juu yake) alisema [Qur'an 3:51],

"Hakika Allah ndiye Mola wangu na Mola wenu, basi muabuduni Yeye pekee. Hii ndiyo Njia Iliyo Nyooka."

Muhammad (rehma na amani iwe juu yake) alisema [Qur'an 18:110],

"Imenifunulia kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja. Basi anayetarajia kukutana na Mola wake, na atende mema na asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake."

Ujumbe huu ulikuwa thabiti katika vizazi vyote, na unasisitiza umuhimu wa kuwa na imani sahihi kwa Mwenyezi Mungu.

Kila Taifa Lilitumiwa Nabii

"Kwa kila taifa kuna mjumbe." Qur'an 10:47

Waislamu wanaamini kuwa maelfu ya Manabii walitumwa mara kwa mara na Allah, angalau mmoja kwa kila taifa, kama rehema kwa wanadamu kwa ajili ya mwongozo wao. Katika hali fulani, ujumbe wa Manabii ulipotea, kuharibiwa, kusahaulika, kupuuzwa, au kukataliwa na watu. Hizi zilikuwa baadhi ya sababu kwamban Nabii mpya alitumwa kufikisha upya ujumbe wa Allah.

Waislamu wanaamini na kuwaheshimu kila Nabii aliyetumwa na Mwenyezi Mungu. Waislamu pia wanaamini vitabu vyote vya mbinguni vilivyoteremshwa kwa Manabii, wakijua kwamba hakuna hata kimoja kinachopatikana leo katika hali yake ya awali, isipokuwa Qur'an.

"Ni Yeye (Allah) ambaye amekuteremshia Kitabu (Qur'an) kwa haki, kuthibitisha yale yaliyotangulia. Na aliteremsha Taurati na Injili." Qur'an 3:3

Kwa nini kila mtu hapokei Ufunuo wa Moja kwa Moja?

Allah aliumba maisha na kuwapa wanadamu hiari ya kuchagua kwa akili, kama mtihani ili kuona ni nani atakayefuata njia Yake kwa hiari na ni nani atakayetoka. Ikiwa kila mtu angepokea ufunuo wa moja kwa moja kutoka kwa Allah, maisha yasingekuwa mtihani wa kweli wa imani. Mtihani halisi wa imani ni kutumia akili na fikra kutafakari na kutambua ishara za Mwenyezi Mungu, badala ya kuzungumza moja kwa moja na Mwenyezi Mungu, jambo ambalo halingehitaji juhudi yoyote na lingefanya imani isiwe na maana.

Ingawa Manabii walipokea ufunuo wa moja kwa moja, hilo halikuwazuia kukabiliana na mitihani ya maisha, kwani Utume unakuja na changamoto nyingi na majaribu makubwa.

Nabii wa Mwisho

Manabii walitumwa kwa makundi maalum ya watu, na kwa muda ujumbe waliokuja nao ulipotea au kuharibiwa. Lakini Mtume Muhammad (rehma na amani iwe juu yake) hakutumwa kwa kundi maalum la watu, bali kwa wanadamu wote, na ujumbe wake umehifadhiwa katika Qur'an na Sunnah.

Kwa kuwa Qur'an na Sunnah vimehifadhiwa na ni rahisi kupatikana, hakuna haja ya Nabii mwingine.

· Qur'an ni neno la Allah lililonenwa, na halina upotovu, makosa au migongano yoyote. Ni kitabu cha "uongozi kwa wanadamu... na kipambanuzi (kati ya haki na batili)." Qur'an 2:185

· Sunnah ni mkusanyiko wa maneno na matendo ya Mtume Muhammad (amani iwe juu yake), kama ilivyorekodiwa na maswahaba wake na wanafunzi wao. Na ukweli kwamba kuna maelfu ya hizi zilizorekodiwa na kuthibitishwa kwa umakini hufanya iwe rahisi kwa mtu yeyote kumfuata Mtume Muhammad (amani iwe juu yake) kwa usahihi.

Ujumbe wa Mtume Muhammad uko katika upatanifu kamili na mafundisho ya Manabii waliomtangulia, na unathibitisha ujumbe wao.

Mtume Muhammad (rehma na amani iwe juu yake) ni Mtume wa mwisho kwa wanadamu wote tangu wakati wake hadi mwisho wa wakati, wakiwemo vizazi vya sasa na vijavyo. Alikuwa mfano kamili wa mwanadamu mwaminifu, mwenye haki, mwenye huruma, mwenye upendo, mkweli na shujaa. Kama ilivyokuwa kwa Manabii waliomtangulia, hakuwa na sifa yoyote mbaya, na alijitahidi pekee kwa ajili ya Allah.

Hitimisho

"Kwa hakika katika Mtume wa Allah [Muhammad] kuna mfano mwema wa kuigwa kwa yule anayemtarajia Allah na Siku ya Mwisho, na anamkumbuka Allah kwa wingi." Qur'an 33:21

Manabii walitumwa kama rehema kutoka kwa Allah, kufikisha ujumbe Wake na kuwafundisha watu jinsi ya kuishi maisha ya ucha Mungu. Wana sifa bora kabisa, na wanapaswa kufuatwa na kutiiwa.

Kumfuata Nabii ni utiifu kwa Allah, na kumkataa Nabii ni uasi dhidi ya Allah. Mtume Muhammad (rehma na amani iwe juu yake) ni Mtume wa mwisho, hivyo uongofu wa Allah ulikamilika kwa kuja kwake, na wokovu wetu unakamilika kwa kumtii Allah na Nabii Wake wa mwisho.

Similar Downloads

No related download found!