Description
Yesu: Nabii wa Mwenyezi Mungu
Waislamu Wanampenda Yesu
Yesu ni mtu anayependwa na kuheshimiwa na mabilioni ya watu kote ulimwenguni, lakini kuna mkanganyiko mwingi kuhusu hadhi ya utu huu mkubwa. Waislamu na Wakristo wote wanamheshimu Yesu, lakini wanamuona kwa njia tofauti kabisa.
Kijitabu hiki kinakusudia kufafanua masuala yanayo husiana na Yesu: Je, Yesu alikuwa Mungu, au alitumwa na Mwenyezi Mungu? Yesu alikuwa nani? wa kihistoria wa kweli?
Yesu Kama Mwenyezi Mungu
Baadhi ya Wakristo wanadai kwamba "Yesu ni Mungu" au sehemu ya Utatu Mtakatifu - kwamba yeye ni mwili wa Mwenyezi Mungu duniani, na kwamba Mungu alichukua umbo la kibinadamu. Hata hivyo, kulingana na Biblia, Yesu alizaliwa, alikula, alilala, alisali, na alikuwa na maarifa yenye mipaka – sifa zote ambazo hazifai kwa Mungu. Mwenyezi Mungu ana sifa za ukamilifu, ilhali mwanadamu ni kinyume chake. Inawezekanaje kitu kuwa na sifa mbili zinazopingana kikamilifu na mapungufu kwa wakati mmoja?
Uislamu unafundisha kwamba Mwenyezi Mungu ni mkamilifu daima. Kuamini kwamba Mungu alikua mwanadamu ni kudai kwamba Mungu alikuwa (au wakati fulani alikuwa), si mkamilifu. Mkristo anapaswa kujiuliza, je, wazo la mungu ambaye kwa wakati mmoja alikuwa mtoto dhaifu asiyeweza kuishi bila chakula, kinywaji au usingizi linaweza kuwa sawa na Mwenyezi Mungu i anayesifiwa kwenye Agano la Kale? Bila shaka hapana.
Mtu anaweza kuuliza, "Kama Mwenyezi
Mungu anaweza kufanya chochote, kwa nini hawezi kuwa mwanadamu?"
Kwa ufafanuzi, Mungu hafanyi matendo yasiyolingana na uungu Wake. Mwenyezi Mungu hafanyi jambo lolote litakalomfanya awe kitu tofauti na Mungu. Kama Mungu angekuwa mwanadamu na kuchukua sifa za kibinadamu, angeacha kuwa Mungu kwa lazima.
Baadhi ya sehemu isiyoeleweka vizuri katika Biblia inaweza kutumiwa vibaya kuonyesha kwamba Yesu ni wa kiungu kwa njia fulani. Lakini tukitazama sehemu za wazi katika Biblia, tunaona tena na tena kwamba Yesu anatajwa kama binadamu wa kipekee na si zaidi ya hayo. Biblia ina sehemu nyingi ambapo Yesu anazungumza na kutenda kana kwamba Mwenyezi Mungu ni kiumbe tofauti na yeye mwenyewe. Kwa mfano:
· Yesu "alianguka kifudifudi na kuomba." [Mathayo 26:39] Ikiwa Yesu alikuwa Mungu, je, Mwenyezi Mungu angeweza kuanguka kifudifudi na kuomba? Na alikuwa anaswali kwa nani?
· Biblia inamwita Yesu Nabii [Mathayo 21:10-11], kwa hivyo Yesu angewezaje kuwa Mungu na Nabii wa Mwenyezi
· Mungu kwa wakati mmoja?
· Yesu alisema, "Ninaenda kwa Baba, kwa sababu Baba ni mkuu kuliko mimi." [Yohana 14:28]
· Yesu alisema, "Ninapaa kwa Baba yangu na Baba yenu, na kwa Mungu wangu na Mungu wenu." [Yohana 20:17] Ikiwa Yesu alikuwa Mungu, kwa nini aseme "kwa Mungu wangu na Mungu wenu," na alikuwa akipaa kwa nani?
Ikiwa Yesu alikuwa Mungu, angewaambia watu waziwazi wamwabudu, na kungekuwa na sehemu ya wazi katika Biblia inayosema hivyo; lakini alifanya kinyume na akakataa mtu yeyote kumwabudu: "Na bure wananiabudu." [Mathayo 15:9]
"Mwana wa Mungu"
Wakristo wengine wanadai kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. Hili linamaanisha nini hasa? Hakika Mungu yuko mbali na kuwa na mwana wa kimwili na wa moja kwa moja. Binadamu wanapata watoto wa kibinadamu. Paka wanapata vitoto vya paka. Je, inamaanisha nini kwa Mwenyezi Mungu kuwa na mtoto?
Badala ya kuchukuliwa kwa maana halisi, tunaona neno "Mwana wa Mungu" linatumika kwa njia ya mfano katika lugha za zamani za Biblia kumaanisha "mtu mwadilifu," na limetumika kwa Daudi, Sulemani, na Israeli - si kwa Yesu pekee: "...Israeli ni mzaliwa wangu wa kwanza" (Kutoka 4:22). Kwa kweli, mtu yeyote mwadilifu anaitwa "mwana wa Mungu": "Wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu ni wana wa Mungu." [Warumi 8:14]
Kijisehemu:
"Haistahiki kwa (utukufu wa) Mwenyezi Mungu kwamba
apate mwana. Yeye ni Mkamilifu na Asiye na dosari! Anapoamua jambo, huliambia tu 'Kuwa' na linakuwa." [Qur'an 19:35]
"Baba na Bwana"
Vivyo hivyo, neno "Baba" linapotumiwa kumrejelea Mungu, halipaswi kuchukuliwa kwa maana halisi. Badala yake, ni njia ya kusema kwamba Mungu ni Muumba, Mlezi, na Mola Mkuu wa vyote. Kuna aya nyingi zinazotusaidia kuelewa maana ya mfano ya neno "Baba," kwa mfano: "Mungu mmoja na Baba kwa wote." [Waefeso 4:6]
Pia, Yesu wakati mwingine alitwa 'Bwana' na wanafunzi wake. Neno hili hutumika katika lugha za asili za Biblia kwa Mungu na pia kwa watu wanaoheshimiwa sana. Kwa mfano, katika Agano Jipya la Kiyunani, neno kyrios linatumika kwa 'Bwana' na pia kumrejelea mmiliki wa shamba la mizabibu (Mathayo 20:8), na bwana aliyempiga mtumishi mkaidi (Luka 20:42-47).
Katika sehemu nyingine za Biblia, Yesu anaitwa "mtumishi wa Mungu "na wanafunzi: "Mungu wa baba zetu amemtukuza mtumishi wake Yesu." [Matendo 3:13] Hii inaonyesha wazi kwamba neno 'Bwana' linapotumika kumrejelea Yesu, ni cheo cha heshima, si cha uungu.
Jaribio linafanywa kufafanua ugumu wa masuala haya kuhusu asili ya Mungu na asili ya Yesu, ambayo mara nyingi huleta mkanganyiko au kutoridhisha. Lakini jambo kuu la kutafakari ni: Kwa nini Mungu afanye iwe vigumu sana kuelewa? Je, mafundisho haya magumu yanalinganishwaje na mafundisho ya Uislamuambayo ni rahisi, wazi, na safi yanayoelezea dhana ya Mwenyezi Mungu?
Yesu: Nabii
Katika Uyahudi, Yesu (amani iwe juu yake) anakataaliwa kama Masihi. Hii inapingana waziwazi na Ukristo ambako anaheshimiwa kama mungu au mwana wa Mungu. Uislamu unachukua msimamo wa kati na kumkubali Yesu kama Nabii mwenye heshima na Mjumbe wa Mungu, vilevile Masihi, lakini Waislamu hawamuabudu - kwani ibada ni kwa Mwenyezi Mungu pekee aliyemuumba Yesu na kila kitu kilichopo.
"[Yesu] alisema: 'Hakika mimi ni mtumwa wa Mwenyezi Mungu. Amenipa Kitabu na kunifanya kuwa Nabii.'" [Qur'an 19:30]
Kuzaliwa kwa Muujiza
Kulingana na Qur'an, Malaika Jibril alitumwa kwa Mariamu, bikira mtukufu, kwa sura ya mwanamume, akimjulisha juu ya mtoto ambaye atakayezaliwa kwa muujiza bila baba.
"Akasema [Malaika Jibril]: 'Hakika mimi ni mjumbe wa Mola wako, ili nikutangazie zawadi ya mtoto mwema.' Akasema: 'Nitapataje mtoto hali hakuna mwanamume aliyenigusa, wala mimi si mwovu?' Akasema: 'Hivyo ndivyo itakavyokuwa. Mola wako amesema: “Ni rahisi kwangu, na tutamfanya kuwa ishara kwa watu na rehema itokayo Kwetu. Na jambo hili limekwisha amriwa.”' [Qur'an 19:19-21]
Wengine wanadai kuwa kuzaliwa kwake kwa muujiza ni ushahidi wa uungu wa Yesu. Hata hivyo, Yesu hakuwa wa kwanza kuumbwa bila baba, kwani Nabii Adam (amani iwe juu yake) kabla yake hakuwa na baba wala mama. Mungu anasema:
"Hakika mfano wa Yesu mbele ya Mungu ni kama wa Adam; Alimuumba kutoka kwenye udongo, kisha akamwambia: 'Kuwa,' naye akawa. Huu ni ukweli kutoka kwa Mola wako, kwa hivyo usiwe miongoni mwa wenye shaka." [Qur'an 3:59-60]
Ikiwa Yesu anaabudiwa kwa sababu hakuwa na baba, basi hakika Adam anastahili kuabudiwa zaidi kwani aliumbwa bila baba wala mama.
Miujiza ya Yesu
Yesu alizaliwa kwa muujiza bila baba na alifanya miujiza mikubwa kwa idhini na matakwa ya Mwenyezi Mungu.
Alizungumza akiwa mtoto mchanga kitandani ili kumtetea mama yake dhidi ya wale waliomtuhumu kwa uzinzi. Qur'an pia inasema kwamba Yesu aliwafufua wafu, aliponya wenye ukoma na vipofu - yote kwa matakwa ya Mwenyezi Mungu.
Ukweli kwamba Yesu (amani iwe juu yake) alifanya miujiza haimaanishi kwamba alikuwa zaidi ya mtumwa mnyenyekevu wa Mungu. Kwa kweli, Mitume wengi walifanya miujiza, wakiwemo Nuhu, Musa, na Muhammad (amani iwe juu yao wote), na miujiza hii ilitokea tu kwa idhini ya Mungu ili kuthibitisha ukweli wa Mtume.
Ujumbe wa Yesu
Manabii wa Agano la Kale kama vile Ibrahimu, Nuhu na Yunus hawakufundisha kwamba Mungu ni sehemu ya Utatu, wala hawakumwamini Yesu kama mwokozi wao.
Ujumbe wao ulikuwa rahisi: kuna Mungu mmoja tu na Yeye pekee anastahili kuabudiwa. Si jambo lenye mantiki kwa Mwenyezi Mungu kutuma Manabii kwa maelfu ya miaka na ujumbe uleule wa msingi, kisha ghafla aufanye tofauti, adai kuwa sasa Yeye ni sehemu ya Utatu, na kulazimisha imani katika uungu wa Yesu ili kuokolewa.
Ukweli ni kwamba Yesu alihubiri ujumbe uleule kama Manabii wote wa Agano la Kale. Kuna sehemu katika Biblia inayosisitiza ujumbe huu wa msingi. Mtu alimjia Yesu na kumuuliza, “Amri ya kwanza ni ipi?” Yesu akajibu, “Amri ya kwanza ni hii: Sikia, Ee Israeli, Bwana Mungu wetu ni Mungu mmoja.” [Marko 12:28-29] Hivyo, amri kuu, imani muhimu zaidi kulingana na Yesu, ni kwamba Mungu ni mmoja. Ikiwa Yesu alikuwa Mungu, angesema: 'Mimi ni Mungu, niabuduni.' Badala yake, alirudia tu aya kutoka Agano la Kale kuthibitisha kwamba Mungu ni Mmoja.
Hii inalingana na ujumbe wa Yesu kama ulivyofundishwa katika Uislamu, ambapo Yesu alitumwa kwa Wana wa Israeli kuthibitisha ujumbe wa Manabii wa zamani - kuamini katika Mungu Mmoja wa Kweli.
"Na alipokuja Yesu na hoja zilizo wazi, alisema: ... Hakika Mwenyezi Mungu - Yeye ni Mola wangu na Mola wenu. Kwa hivyo muabuduni Yeye peke yake. Huu ndio Njia Iliyonyooka." [Qur'an 43:63-64]
Kama Mjumbe mtukufu na mtiifu wa Mwenyezi Mungu, Yesu alijisalimisha kwa hiari kwa amri za Mwenyezi Mungu. Kwa hivyo, alikuwa "Muislamu" - neno linalomaanisha yeyote anayejisalimisha kwa matakwa na amri za Mwenyezi Mungu.
Yesu katika Uislamu
Yesu alikuwa Nabii mtukufu aliyetumwa na Mwenyezi Mungu kuwaita watu kumuabudu Mwenyezi Mungu pekee.
Hili linaonekana wazi katika Biblia na kuthibitishwa katika Qur'an. Imani ya Kiislamu kuhusu Yesu inaeleza Yesu halisi alikuwa nani, huku ikidumisha imani safi kuhusu Mwenyezi Mungu, ukuu Wake, upekee na ukamilifu Wake.
Tunakualika uchunguze zaidi na uangalie Uislamu. Sio dini nyingine tu. Ni ujumbe uleule uliohubiriwa na Nuhu, Ibrahimu, Musa, Yesu na Muhammad – amani iwe juu yao wote. Uislamu maana yake ni ‘kujisalimisha kwa Mungu’ na ni njia ya maisha ya asili na kamilifu inayomhimiza mtu kuzingatia uhusiano wake na Mungu na uumbaji Wake. Uislamu unafundisha kwamba Mungu ni Mwenye Haki na Mwenye Rehema, na hahitaji kujitoa muhanga ili kusamehe dhambi, wala hakuna mtu anayezaliwa na madhambi Mwenyezi Mungu anawahukumu watu kulingana na matendo yao wenyewe, na kila mtu atawajibika kwa vitendo vyake mwenyewe.
Uislamu unatufundisha kuwapenda na kuwaheshimu Manabii wote wa Mwenyezi Mungu, lakini kuwapenda na kuwaheshimu hakumaanishi kuwaabudu, kwa sababu ibada ni kwa Mwenyezi Mungu pekee. Kukubali Yesu kama Nabii wa Mwenyezi Mungu na kuwa Muislamu haimaanishi kubadilisha au kupoteza utambulisho wako wa Kikristo. Ni kuhusu kurejea kwenye mafundisho ya asili na safi ya Yesu.
